Wednesday, March 15, 2006

Nani anasema JK hayawezi?


Mwanablogu Reginald Simon Miruko ndiye kanitumia picha hii. Miss Personality, Witness Manwingi, ambaye alikuwa mwakilishi wa Tanzania katika shindano la kumtafuta Miss Tourism wa Dunia mwaka 2006 anasalimia Rais Jakaya Kikwete wakiwa wamekumbatiana. Wote wanatabasamu, wanapendeza na wameshikana VIZURI! Au nimeshindwa kuitafsiri barabara?

Monday, March 13, 2006

Kikwete, CCM na mapato haramu

MAJUZI, Rais Jakaya Kikwete alikutana na 'wafadhili' wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), jijini Dar es Salaam, waliokisaidia kupata pesa za kampeni mwaka 2005. Katikakuzungumza nao, Kikwete alisisitiza mambo mawili. Kwanza, aliwaomba wana CCM wasilewe ushindi walioupata mwaka 2005, badala yake wajiandae kwa uchaguzi mkuu ujao wa mwaka 2010. Hii ni changamoto nzuri kutoka kw amtu anayetarajiwa kuwa mwenyekiti wa chama hicho katikati ya mwaka huu. Pili, aliwaasa wanachama wenzake waanze kutafakari namna ya kupata MAPATO HALALI kwa ajili ya kampeni. Hili ndilo linazua maswali, hasa kwa kuwa limesemwa sasa baada ya chama kushinda kwa nguvu kubwa ya pesa, huku kikiwa kinashutumiwa kusaidiwa na matajiri kadhaa wanaojihusisha na ujambazi. Je, Kikwete anakiri kwamba ameingia madarakani kwa kutumia pesa haramu? Na je, vyanzo haali vikikosekana, au kama havitatosha, CCM itapataje ushindi? Au itarudi kule kule?! TUJADILI.

Monday, March 06, 2006

Waandishi katika mjadala mzito


KUNA mjadala umeibuka. Ulianzia Bungeni Dodoma, katika kikao cha pili cha Bunge hilo, cha Februari 2006. Mwandishi wa zamani, ambaye sasa ni mwanasheria na mbunge wa Kyela, Dk. Harrison Mwakyembe, alichokoza nyuki pale alipojenga hoja kwamba Bunge liazimie kuibana serikali iwasomeshe waandishi kwa kuwa baadhi yao, kama si wengi wao, hawana elimu ya kutosha, uandishi unabadilika na kukua kila mara na kwamba jukumu hili hawawezi kuachiwa wamiliki wa vyombo vya habari. Alitumia kila msamiati aliodhani kwamba ungemsaidia kujenga hoja na kuonyesha kwamba KUNA TATIZO. Maskini Dk. Mwakyembe, hakujua kwamba alikuwa anachokoza nyuki. Waandishi walichukia, na wengi wao sasa wamekuwa wakimshambulia magazetini kwa madai kwamba aliwatukana kuwaambia hawajasoma.Baadhi yao wanataka awaombe radhi. Wengine wamefikia hata kuazimia kutokuandika habari zake. Nawe u miongoni mwao? Una maoni gani? Soma hapa kwanza, upate maoni yangu. Soma na hii hapa.
My photo
Nimechongwa na mambo haya: Falsafa, Fasihi, Muziki, Habari na Harakati. Sifuati mkumbo. Napenda kuhoji na kudadisi - hulka ya kifalsafa ya kuusaka ukweli - 'UKWELI ULIO UCHI.'