Monday, July 18, 2011

Goli la ajabu

Unalionaje goli hili la penalti ya kisigino?

Ufsiadi wa nguzo ya umeme


Kwa jinsi hii mgawo utaisha?

Monday, May 02, 2011

Obama azungumzia kifo cha Osama

Nukuu ya leo kutoka kwa Rais Barack Obama wa Marekani: "Hatupigani vita dhidi ya Uislamu kwa sababu Bin Laden si kiongozi wa Uislamu... na ameua maelfu ya Waislamu." Sikiliza hotuba ya Rais Obama, akitangaza kifo cha Osama Bin Laden..

Na licha ya makundi ya watu kudai kwamba Marekani inasema uwongo, haijamuua Osama, mtandao wake wenyewe, Al-qaeda, umekiri kwamba bosi wao kafa.

Wednesday, February 23, 2011

Ni kweli! Tatizo si Dowans, ni serikali

Kwa wanaofuatilia mjadala kuhusu Dowans wiki hii, ndugu yangu Absalom Kibanda ameandika kwenye bidii baada ya kusoma maoni yangu na ya Kitila Mkumbo. Sisi tumesema mwenye tatizo si Dowans bali watawala wetu na washauri wao; maana tunaweza kujikuta tunaacha kupamabana na waliotusababishia matatizo, tunabaki kukabana koo na wawekezaji ambao wameletwa tu - na wao wanatafuta kila upenyo wa kibiashara. Kibanda amefafanua vizuri zaidi hoja hii, nami nikaona niwawekee wasomaji wa blogu hii. Ameandika hivi:

"Kitila/Ansbert

Nimewaelewa, mmetufikirisha. Tunamuacha adui na kumshambulia mhanga. Hiyo ndiyo siri ambayo Kikwete na serikali yake wanaificha. Wanatambua kwamba wao ndiyo wenye makosa, wanatambua kwamba makosa waliyofanya katika mkataba wa Richmond ndiyo yaliyotufikisha hapa tulipo leo. Leo hii wanashangilia chini chini na waziwazi wanapoona waandishi wa habari, wanazuoni na wachambuzi wa mambo wakielekeza mashambulizi yao kwa Dowans wakati ukweli ukiwa bayana kwamba tunaopaswa kuwawajibisha ni viongozi wetu serikalini ambao wameitumia sekta ya nishati na madini kama mtaji wa mapato yao haramu.

Hivi nani hajui kuwa ufisadi kupitia mikataba ya IPTL na Songas ni wa kutisha kuliko ilivyo kwa Dowans. Hivi Watanzania wangapi wanajua kwamba fedha ambazo Taifa hili lilikopwa na Benki ya Dunia tena kwa riba ndizo tuliipa kampuni iliyoanza uwekezaji wa Songas kuwekeza kama mtaji wake wa asilimia 100 halafu baada ya sisi kuwapa mtaji huo kampuni hiyo ikafanikisha uwekezaji huo haramu na leo wanatuuzia umeme na deni la WB tunalipa.

Nani amesahau uharamia wa IPTL ambao ulikaribia kumpokonya maisha (Patrick) Rutabanzibwa aliyejaribu kupinga uwekezaji wake? Nani anaikumbuka ile story ya The Ugly Malaysians iliyoandikwa kueleza siri ya ufisadi wa kutisha ndani ya IPTL. Nani hajui kwamba gharama ambazo serikali inatumia kuigharamia IPTL kwa mwezi mmoja zinaendesha mitambo ya Dowans kwa miezi minne?

Hivi kama tungekuwa tumewekeza katika sekta ya nishati ipasavyo tulikuwa na sababu ya kuwaita wawekezaji wa msimu wa aina ya Dowans, IPTL na Songas? Ni serikali gani kama si hizi za CCM ambazo ndizo zimetufikisha hapa?

Hivi Kikwete ambaye alikaa katika Wizara ya Nishati na Madini kwa miaka mingi akiwa Naibu Waziri na Waziri kamili alifanya nini cha maana kulinusuru taifa na matatizo ya leo? Kama alishindwa akiwa katika wizara mama ataweza akiwa rais? Kwa nini hatulishangai hilo?

Kwa nini hatujiulizi? Iweje akiwa Ikulu ameshindwa kubaini mianya ya ufisadi katika umeme wa dharura wakati yeye mwenyewe akiwa ndiye aliye na siri nzito kuhusu kuwapo kwa IPTL hapa nchini? Mbona viongozi wetu wanatumia wepesi wa Watanzania kusahau kwa manufaa yao?

Ni kwa sababu ya jeuri hiyo ndiyo maana leo anadiriki kusema hawafahamu wamiliki wa Dowans. Ni kwa sababu hiyo ndiyo maana ni yeye aliyewapa baraka AG (Frederick) Werema na (Waziri wa Nishati na Madini) William Ngeleja kutamka kwamba tutawalipa Dowans na baada ya akina Sitta, Mwakyembe na wanaharakati wengine kuibuka na kumtisha akageuka na kusema eti naye ni mmoja wa watu ambao hawapendi Dowans walipwe.

Ni yeye aliwapa baraka awali akina Dk. Idris Rashid na Ngeleja za kutaka serikali inunue mitambo hiyo ya Dowans na halafu joto lilipozidi kupinga msimamo huo akageuka na kusema eti uamuzi wao wa kuachana na nia yao ya kuinunua ilikuwa ni wa kusoma alama za nyakati. Je ni haki kumuacha huyu na serikali yake salama na kumshambulia Adawi na Dowans yake? Tunapaswa kufikiri upya.

Ndiyo maana baadhi yetu tunachelea kuiunga mkono CCM na serikali yake. ndiyo maana huwa nawashangaa baadhi ya viongozi wa upinzani wanapohadaika na kuwaunga mkono wahuni kadhaa wa ndani ya CCM wanaojifanya wazalendo wakati rekodi zilizo wazo zikithibitisha pasipo shaka kwamba hao ni maruhani wanaoifanyia kazi CCM kwa staili ya kuuhadaa umma."

Tuesday, February 22, 2011

Adawi apigwa picha


BAADA ya sokomoko la juzi la Brig. Jenerali Sulaiman Mohammed Yahya Al-Adawi kukataa kupigwa picha, leo "zimefanyika njama kinamna" dhidi yake, akapigwa picha bila kujua alipokuwa anatembelea mitambo yake ya Dowans Ubungo, Dar es Salaam. Ndiye huyu hapa! Na baada tu ya ziara yake hiyo, akaelekea uwanja wa ndege kupanda pipa kurudi makwao Oman. Hata hivyo, kabla ya tukio hilo la Ubungo, Adawi alimtembelea Makamu wa Rais Dk. Gharib Bilal, Ikulu, na akiwa ofisini kwa makamu wa rais, alikataa katakata kupigwa picha yoyote kama alivyowagomea waandishi juzi.

Sunday, February 20, 2011

Mmiliki wa Dowans yuko Bongo








Mmiliki wa Dowans, Brigedia Jenerali (Mstaafu) Sulaiman Mohammed Yahya Al Adawi, anayeishi Oman, ametua nchini na kuzungumza na vyombo vya habari katika hoteli ya Kilimanjaro Kempinski, Dar es Salaam. Akiwa na wakurugenzi wawili Stanley Munai na John Miles, alisema amelazimika kuja kwa sababu amesikia watu wanadai hawamjui mmiliki wa Dowans, na kwamba wanawadhania baadhi ya Watanzania kuwa ndio wamiliki wa Dowans. Akasema: "Mimi ndiye mmiliki wa Dowans."

Akasema si kawaida yake kuzungumza na vyombo vya habari, na kwamba hataki kupigwa picha yoyote, kwa sababu yeye ni mfanyabiashara asiyependa makuu na asiye na makeke. Akasema amewekeza katika nchi 12 duniani, na kwamba katika zote hizo anawakilishwa na rafiki zake; na kwamba hapa nchini aliletwa na Rostam Aziz mwaka 2005 kwa ajili ya mradi wa Fibre Optic.

Katika hili la sasa, alisema amekuja kujadiliana na Tanesco juu ya hatima bora ya kibiashara kwake na fursa ya umeme kwa Watanzania, katika mazingira ya sasa ya mkataba unaodaiwa kuwa na utata, na deni la bilioni 94 analoidai Tanesco baada ya Dowans kuwashinda Tanesco mahakamani. Alizungumza kwa Kiingereza, na nimeweza kunukuu baadhi ya kauli zake moja kwa moja alipokuwa akijibu baadhi ya maswali na hoja za waandishi. Hizi hapa:

1. “I am here to find a happy resolution, a business decision. I am ready to offer something nice to Tanesco if it works out.”

2. “I don’t want to be known. I am a low-profile businessman. I walk free here in Dar es Salaam, and no one knows I own Dowans.”

3. “Rostam Azizi is a friend of mine. He invited me to come and invest here, but he didn’t put in any cent in the project.”

4. “I have businesses in 12 countries allover the world. I can’t go and represent myself in every country. That’s why I gave Rostam power of attorney.”

5. “We have not been tarnished, but we have been mixed up with something else (Richmond)”

6. “I do not need to be cleared by anyone; my electricity here will clear me.”

Friday, February 11, 2011

Kikwete anawajua Dowans

HOJA yangu ni kwamba Rais Jakaya Kikwete na serikali yake wanawajua Dowans kabla hata hawajarithi mkataba wa Richmond. Wanajua kuwa wanasheria wetu ndio walioandika mkataba huo; ndio waliotushauri kuuvunja; na ndio waliotutetea tukashindwa. Kauli ya sasa ya Rais Kikwete kwamba hawajui Dowans ni ya kujikosha, na ya kisaliti kama ya Mtume Petro, mbele ya kijakazi, dhidi ya Yesu. Blogu hii inajua kuwa Rais Kikwete alishiriki kuwabeba wawekezaji hao, hasa baada ya matatizo yaliyosababishwa na Richmond. Na blogu hii inajua kuwa Rais Kikwete anataka Dowans walipwe pesa zao, lakini anakosa ujasiri kwa sababu za kisiasa. SOMA Maswali Magumu hapa.

Friday, January 07, 2011

Mkanganyiko wa risasi za moto dhidi ya raia Arusha

KATIKA taarifa ya jana, Polisi Mkoani Arusha walisema wameua watu wawili tu; baadhi ya vyombo vya habari, kikiwamo BBC, vikadai wamekufa watu wapatao 10. Polisi wakadai walipiga risasi watu sita (6) tu, lakini viongozi wa Chadema walipoachiwa na mahakama wakaenda kutembelea majeruhi hospitalini, walikuta wananchi wapatao 38 wote wana majeraha ya risasi. Chadema wakaunda kamati ya kuwahudumia majeruhi hao. Sasa inadaiwa polisi wamekula njama na uongozi wa hospitali hiyo ya Mount Meru, wamewatorosha majeruhi hao, hawajulikani walikopelekwa, ili kuficha ukweli kuhusu idadi ya waliojeruhiwa kwa risasa. Viongozi wa Chadema wanaendelea kufuatilia. Tusipochunga, taratibu, Tanzania itageuka Police State!

Ajabu ni kwamba Polisi hawajawakamata polisi hao walioua raia; badala yake wanawakamata raia waliokuwa wanatembea kwa miguu (wanaandamana sio?) kuelekea mkutanoni.
My photo
Nimechongwa na mambo haya: Falsafa, Fasihi, Muziki, Habari na Harakati. Sifuati mkumbo. Napenda kuhoji na kudadisi - hulka ya kifalsafa ya kuusaka ukweli - 'UKWELI ULIO UCHI.'