Tuesday, April 04, 2006

Serikali Kusomesha Waandishi

MALUMBANO kati ya waandishi na Dk. Harrison Mwakyembe, na kati yake na serikali kupitia Bunge, juu ya wajibu wa serikali kusomesha waandishi sasa yamepata mwelekeo. Soma stori hii hapa chini:

SERIKALI imekubali ushauri wa Mbunge wa Kyela, Dk. Harrison Mwakyembe, kuwasomesha waandishi wa habari na kutunga sheria zinazolinda taaluma na maslahi yao.

Katika majibu ya maandishi kwa mbunge huyo, Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, Muhammad Seif Khatib, amesema serikali itaandaa programu ya kutoa mafunzo kwa waandishi wa habari yanayolenga elimu ya juu.

“Majukumu makubwa ya wizara katika programu hiyo ni kuratibu upatikanaji wa misaada kwa ajili ya mafunzo ya muda mfupi, muda wa kati na ya muda mrefu ndani na nje ya nchi.

“Katika programu hiyo, wamiliki wa vyombo vya habari watatakiwa kuandaa orodha za wanahabari wanaohitaji mafunzo, na kuchangia gharama za mafunzo hayo.”

Kwa sababu hiyo, waziri alisema serikali itaandaa rasimu ya sheria inayotekeleza maelekezo ya Sera ya Habari na Utangazaji ya mwaka 2003.

Kwa majibu wa maelezo ya waziri, sheria hiyo itaunda chombo ambacho kitalinda na kutetea taaluma na maadili ya habari.

Serikali pia imesema itaandaa programu ya mafunzo yatakayowawezesha waandishi kubobea katika maeneo maalumu.

“Lengo la programu hii ni kuipatia serikali sekta ya habari wanahabari wenye taaluma za uchumi, kilimo, uhasibu, sheria, utamaduni na michezo,” alisema waziri.

Majibu ya Seif Khatib kwa Dk. Mwakyembe ni sehemu ya majibu mengine yanayotolewa na serikali kwa hoja za wabunge kama ilivyoagizwa na Waziri Mkuu, Edward Lowassa.

Katika hoja yake ya msingi, kwenye kikao cha pili cha bunge kilichopita, Dk. Mwakyembe alishauri serikali iweke utaratibu wa kuwasomesha waandishi ndani na nje ya nchi, itenge walau nafasi 10 hadi 20 kwa mwaka (kuanzia mwaka huu), ili waandishi nao wapate fursa ya kujiendeleza kielimu na kubobea katika taaluma yao kama walivyo wanataaluma wengine.

Alisema hatua hiyo itapunguza baadhi ya manung’uniko yanayotokana na makosa ya kitaaluma, na kuongeza ujuzi na uelewa katika masuala yanayoandikwa.

Alijenga hoja kwa kusisitiza kwamba baadhi ya waandishi wanafanya kazi hiyo bila kuwa na elimu ya kutosha, na kwamba ni wajibu wa serikali kuwawezesha ili viwango vyao vya elimu viendane na mahitaji ya kitaaluma na zama tulizomo.

Alitoa mfano wa serikali ya Uganda ambayo ilipitisha sheria kuwalazimisha waandishi wasome walau hadi kiwango cha shahada moja; akasema ingawa uamuzi huo uliwatesa na ulilalamikiwa mwanzoni, umekuwa wa manufaa kwa waandishi wa Uganda na jamii yao kwa ujumla.

Aliishauri serikali isilazimike kuchukua uamuzi mgumu kama huo, lakini ianze pole pole kutoa nafasi na kuzilipia katika vyuo vikuu ndani na nje ya nchi. Dk. Mwakyembe alipendekeza kwamba jukumu hili lisiwe la wamiliki wa vyombo vya habari, bali la serikali.

Hoja hiyo haikuwapendeza baadhi ya waandishi; wakadai kwamba mbunge huyo ana jeuri ya usomi, amewatukana kwa kusema hawajasoma vizuri. Baadhi walimuunga mkono wakasema ipo haja ya serikali kuwasomesha waandishi kwa sababu kihistoria imewatelekeza.

Alipoitembelea wizara husika wiki kadhaa zilizopita, Rais Jakaya Kikwete, alichochea hoja kwa kumshauri waziri aweke utaratibu wa kuwaendeleza waandishi kitaaluma.
My photo
Nimechongwa na mambo haya: Falsafa, Fasihi, Muziki, Habari na Harakati. Sifuati mkumbo. Napenda kuhoji na kudadisi - hulka ya kifalsafa ya kuusaka ukweli - 'UKWELI ULIO UCHI.'