Monday, March 31, 2008

Nyerere ataka kijiji, Kikwete mji




Nyerere hakutaka Butiama iwe makao makuu

Na Beldina Nyakeke, Musoma

CHIFU wa Kabila la Wazanaki, Japhet Wanzagi amesema azma ya Rais Jakaya Kikwete kukifanya kijiji cha Butiama kuwa makao makuu ya Wilaya ya Musoma Vijijini, inapingana na mpango wa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.

Wanzagi ambaye pia ni Mwenyekiti wa Ukoo wa Burito Nyerere, amesema mpango wa Mwalimu Nyerere ulikuwa ni kuifanya Butiama kuwa kijiji cha historia, kinyume na azma hiyo ya Rais Kikwete.

Chifu huyo alisema hayo alipozungumza na waandishi wa habari kuhusu kauli ya Rais Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) aliyoitoa wakati wa ufunguzi wa mkutano wa Halmashauri Kuu ya chama hicho kijijini Butiama hivi karibuni.

Wanzagi alisema kimsingi hapingani na azma ya Rais Kikwete ya kutaka kumuenzi Mwalimu Nyerere kwa kufanya mambo mbalimbali, ikiwamo kukifanya kijiji cha Butiama kuwa makao makuu ya wilaya, lakini akasisitiza kuwa anao ushahidi ingawa si wa maandishi ambao kabla ya kifo chake, Mwalimu Nyerere aliwahi kumweleza nia na madhumuni ya kukifanya kijiji hicho kuwa cha kihistoria.

Alisema katika nia hiyo, Mwalimu Nyerere alipendekeza kijiji cha Kiabakari kilicho jirani na Butiama ndio pawe makao makuu ya wilaya.

Wanzagi alisema endapo serikali itaamua kukifanya kijiji hicho kuwa makao makuu ya wilaya, upo uwezekano wa kuchanganya mila na desturi za makabila mbalimbali kijijini hapo kutokana na muingiliano wa watu watakaohamia katika mji huo hali ambayo Mwalimu Nyerere hakupenda iwepo.

"Ninao ushahidi japo si wa maandishi. Na sijui hata kama Mama (Mama Maria) anajua kuwa mzee hakupeda kijiji cha Butiama kuwa mji. Maana aliniambia kuwa Butiama itakapokuwa mji, basi kutakuwepo na muingiliano wa watu wa makabila mbalimbali na kupoteza uasilia wa kijiji chetu ambapo alitolea mfano jiji la Dar es Salaam, ambalo kutokana na muingiliano wa watu, wenyeji wa pale, yaani wazaramo, wamehama na kusogea nje kabisa ya jiji," alisema.

Katika hotuba yake wakati wa ufunguzi wa mkutano wa NEC, Rais Kikwete alisema ili kumuenzi Mwalimu Nyerere, serikali itakapofikia uamuzi wa kuigawa wilaya ya Musoma Vijijini, Butiama lazima kiwe makao makuu ya wlilaya na kuungwa mkono na mkutano huo na kuiagiza serrikali kufanya haraka kutekeleza pendekezo hilo.

Katika hatua nyingine, Chifu Wanzagi, aliitaka serikali kuwawezesha wakulima kwa kuwapa mahitaji muhimu ikiwa ni pamoja na pembejeo ili kuboresha kilimo.

Habari hii nimeichukua kutoka Tovuti ya Mwananchi kwa sababu za kihistoria. Nimeona ni vema iwekwe mahali ambapo hata tukiitaka kufanyia marejeo tutaipata, maana tovuti ya Mwananchi haitunzi habari zilizopita. - Mhariri.

Saturday, March 29, 2008

Mwinyi amtosa Kikwete?


HABARI za uhakika zinasema kuwa baadhi ya marais na mawaziri wakuu wastaafu wa Tanzania wamegoma kwenda Butiama kushiriki vikao vya Kamati Kuu na Halmashauri Kuu (NEC) ya CCM. Siku chache zilizopita, baadhi yao, chini ya Mzee Ali Hassan Mwinyi, walikuwa na kikao cha dharura kujadili namna ya kuinusuru CCM kutoka kwa mafisadi. Rais Mstaafu Benjamin Mkapa na Waziri Mkuu Mstaafu Frederick Sumaye hawakualikwa. Wajumbe wa kikao cha Mwinyi waliazimia kutumia kikao cha Butiama kumlazimisha Rais Jakaya Kikwete achukue hatua mbili muhimu.

Kwanza, atumie mamlaka aliyonayo kuhakikisha vikao hivyo vinawavua uanachama wale wote waliotuhumiwa katika kashfa za EPA na Richmond. Pili, walitaka atumie nguvu hiyo hiyo, kumuondolea kinga Rais Mstaafu, Benjamin Mkapa, ili afikishwe mahakamani kujibu tuhuma zinazomkabili, na aweze kutoa ushahidi katika kesi ya Balozi Costa Mahalu ambaye amemtaja kama shahidi mkuu.

Ushauri walioupata kwa Mzee Joseph Sinde Warioba ni kwamba ikibidi, Mkapa aondolewe kinga kwa muda tu kwa ajili ya kesi ya Mahalu, halafu arejeshewe.

Katika kikao hicho, Mzee Mwinyi aliwashauri wenzake kwamba iwapo Kikwete atakataa kuchukua hatua hizo, itokee vurumai kubwa, hata kama itawalazimu kuivunja CCM na kuwa CCM A na CCM B. Wazo la CCM kuvunjika halikumpendeza Rais Mstaafu wa Zanzibar, Salmin Amour; kwa maelezo kuwa CCM ikivunjika itakuwa faida ya wapinzani, hasa Zanzibar.

Kwa hiyo, walikubaliana kuwa badala ya kuvunja chama, kama Kikwete hakubali ushauri wao, wao watagoma kushiriki kikao hicho. Alipokataa, kama walivyotarajia, wakaamua kutokushiriki.

Hata baada ya kuamua kutokwenda Butiama, hawakumtaarifu mwenyekiti wao (Kikwete). Alitaarifiwa na watu wa protokol walipokuwa wanaandaa usafiri wa wastaafu hao, huku kila mmoja akitoa udhuru wake papo hapo.

Baadhi yao, wakiwamo Mwinyi, Salim Ahmed Salim, Mkapa na Sumaye, wanasemekana kwenda nje ya nchi katika kipindi walichohitajika kwenda Butiama.

Sababu mojawapo ya Kikwete kukataa kuwachukulia hatua mafisadi wa EPA na Rihmond inasemekana ni hatua yake ya kuwalinda (au kuwaogopa) rafiki zake Edward Lowassa na Rostam Azizi ambao ni watuhumiwa wakuu wa Richmond. Na inasemekana sasa Kikwete amelazimika kuanza mkakati mpya wa kumbeba Lowassa, jambo ambalo limezua 'uhasama' kati yake (JK) na Spika wa Bunge, Samuel Sitta.

Kumeguka kwa wastaafu, hasa Mzee Mwinyi, kutoka kambi ya Kikwete, si habari ndogo. Inafikirisha na kuzua maswali magumu juu ya hatima ya chama na uongozi mzima wa Kikwete. Hadi habari hii inaandikwa, wastaafu walioonekana Butiama wakati kikao cha Kamati Kuu kinaendelea ni Rashid Kawawa, John Malecela na Gharib Bilal. Walio Butiama tuletee habari kuhusu Joseph Sinde Warioba na Cleopa Msuya.

Monday, March 17, 2008

Bado Sisi

Wakenya wamepiga hatua ambayo lazima tuionee wivu. Huko nyuma niliwahi kuandika kwamba kama tunatakakufanya mageuzi tujifunze Kenya. Lakini tunahitaji 'injini ya mageuzi'. Kenya walikuwa na injini yao, Raila Odinga. Sisi tunaye mtu wa aina hiyo? Ni nani? Ndiyo! Tunahitaji 'Mbegu ya Haradali'...
My photo
Nimechongwa na mambo haya: Falsafa, Fasihi, Muziki, Habari na Harakati. Sifuati mkumbo. Napenda kuhoji na kudadisi - hulka ya kifalsafa ya kuusaka ukweli - 'UKWELI ULIO UCHI.'