Tuesday, April 04, 2006

Serikali Kusomesha Waandishi

MALUMBANO kati ya waandishi na Dk. Harrison Mwakyembe, na kati yake na serikali kupitia Bunge, juu ya wajibu wa serikali kusomesha waandishi sasa yamepata mwelekeo. Soma stori hii hapa chini:

SERIKALI imekubali ushauri wa Mbunge wa Kyela, Dk. Harrison Mwakyembe, kuwasomesha waandishi wa habari na kutunga sheria zinazolinda taaluma na maslahi yao.

Katika majibu ya maandishi kwa mbunge huyo, Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, Muhammad Seif Khatib, amesema serikali itaandaa programu ya kutoa mafunzo kwa waandishi wa habari yanayolenga elimu ya juu.

“Majukumu makubwa ya wizara katika programu hiyo ni kuratibu upatikanaji wa misaada kwa ajili ya mafunzo ya muda mfupi, muda wa kati na ya muda mrefu ndani na nje ya nchi.

“Katika programu hiyo, wamiliki wa vyombo vya habari watatakiwa kuandaa orodha za wanahabari wanaohitaji mafunzo, na kuchangia gharama za mafunzo hayo.”

Kwa sababu hiyo, waziri alisema serikali itaandaa rasimu ya sheria inayotekeleza maelekezo ya Sera ya Habari na Utangazaji ya mwaka 2003.

Kwa majibu wa maelezo ya waziri, sheria hiyo itaunda chombo ambacho kitalinda na kutetea taaluma na maadili ya habari.

Serikali pia imesema itaandaa programu ya mafunzo yatakayowawezesha waandishi kubobea katika maeneo maalumu.

“Lengo la programu hii ni kuipatia serikali sekta ya habari wanahabari wenye taaluma za uchumi, kilimo, uhasibu, sheria, utamaduni na michezo,” alisema waziri.

Majibu ya Seif Khatib kwa Dk. Mwakyembe ni sehemu ya majibu mengine yanayotolewa na serikali kwa hoja za wabunge kama ilivyoagizwa na Waziri Mkuu, Edward Lowassa.

Katika hoja yake ya msingi, kwenye kikao cha pili cha bunge kilichopita, Dk. Mwakyembe alishauri serikali iweke utaratibu wa kuwasomesha waandishi ndani na nje ya nchi, itenge walau nafasi 10 hadi 20 kwa mwaka (kuanzia mwaka huu), ili waandishi nao wapate fursa ya kujiendeleza kielimu na kubobea katika taaluma yao kama walivyo wanataaluma wengine.

Alisema hatua hiyo itapunguza baadhi ya manung’uniko yanayotokana na makosa ya kitaaluma, na kuongeza ujuzi na uelewa katika masuala yanayoandikwa.

Alijenga hoja kwa kusisitiza kwamba baadhi ya waandishi wanafanya kazi hiyo bila kuwa na elimu ya kutosha, na kwamba ni wajibu wa serikali kuwawezesha ili viwango vyao vya elimu viendane na mahitaji ya kitaaluma na zama tulizomo.

Alitoa mfano wa serikali ya Uganda ambayo ilipitisha sheria kuwalazimisha waandishi wasome walau hadi kiwango cha shahada moja; akasema ingawa uamuzi huo uliwatesa na ulilalamikiwa mwanzoni, umekuwa wa manufaa kwa waandishi wa Uganda na jamii yao kwa ujumla.

Aliishauri serikali isilazimike kuchukua uamuzi mgumu kama huo, lakini ianze pole pole kutoa nafasi na kuzilipia katika vyuo vikuu ndani na nje ya nchi. Dk. Mwakyembe alipendekeza kwamba jukumu hili lisiwe la wamiliki wa vyombo vya habari, bali la serikali.

Hoja hiyo haikuwapendeza baadhi ya waandishi; wakadai kwamba mbunge huyo ana jeuri ya usomi, amewatukana kwa kusema hawajasoma vizuri. Baadhi walimuunga mkono wakasema ipo haja ya serikali kuwasomesha waandishi kwa sababu kihistoria imewatelekeza.

Alipoitembelea wizara husika wiki kadhaa zilizopita, Rais Jakaya Kikwete, alichochea hoja kwa kumshauri waziri aweke utaratibu wa kuwaendeleza waandishi kitaaluma.

18 comments:

mzee wa mshitu said...

Kaka Ngurumo nimeusikia uamuzi huu wa serikali, nadhani watakuwa wamechoka kubania maana tangu waanze kubana miaka hiyo sasa watakuwa wamechoka. Hebu fikiri fani zote zikiwamo za madaktari, walimu, maboharia, wahasibu na zingine chungu mzima ziliruhusiwa kusoma hadi ngazi za juu, Uandishi wa habari Mhhh!

Ndiyo maana ikawa miaka nenda miaka rudi kachuo ni kale kale ka-TSJ na aliyekuwa akikwea zaidi labda ndiye aliyeruka na ka-advanced diploma sasa hebu angalia ndugu yangu hii si ilikuwa noma kweli kweli kwa hakika nadhani sasa itakuwa makini.

Lakini pia ni lazima wajiandae vema maana wanaanda mtego babu kubwa ambao utawaumiza wao wenyewe.

MICHUZI BLOG said...

charahani umenena kweli. hayo yametokea uganda ambapo hupaswi kuitwa mwandishi kama huna japo shahada ya kwanza. m7 aliwaingiza mjini wakasaini wenyewe waandishi, muswada ukapita.

faraja ni kwamba pamoja na kutosoma kwetu lakini chenga twawala (i.e. kupata zawadi za kimataifa; cnn, sadc etc) na wao wapo.

lakini yooote tisa, kitabu muhimu.hasa wanaoingia fani leo wakitaraji kukuta sahani za dhahabu kwenye fani.

Anonymous said...

Ngurumo,
Tunashukuru kwa kutuletea hii habari. Nitaendelea kuipitia mara kwa mara blogu hii.
Londo-Helsinki

Absalom Kibanda said...

Ansbert katika aya ya pili habari yako unasema; "serikali imekubali ushauri wa Mbunge wa Kyela, Dk. Harrison Mwakyembe, kuwasomesha waandishi wa habari na kutunga sheria zinazolinda taaluma na maslahi yao."

Kimsingi nimesikitishwa na mtazamo wako kuhusu suala hilo la Mwakyembe hasa kutokana na namna unavyojenga hoja kwamba, iwapo asingeuliza lile swali bungeni basi waandishi wasingesomeshwa.

Mimi ninavyojua, mkakati wa kupigania nafasi za masomo kwa ajili ya waandishi wa habari ni ajenda ambayo imekuwa ikijengwa kwa muda mrefu na asasi kadhaa zinazojihusisha na masuala ya habari ikiwamo MISA-Tan ikiongozwa na watu kama akina Salva.

Serikali imemjibu Mwakyembe ikimweleza tu kwamba kile alichokiuliza bungeni tayari kilikuwa kimefanyiwa kazi kwa muda mrefu na serikali na si kwamba kimeamuliwa majuzi baada ya huyo Mwakyembe kuuliza swali bungeni.

Naamini Mwakyembe alipopata hiyo barua ya majibu kutoka serikalini, kwa kutambua uwezo wetu waandishi katika kupambanua mambo akaamua kukutafuta na kukutumia akijitapa kwamba yeye ndiye aliyewezesha hilo likatendeka. Naamini unajua kwamba maamuzi ya namna hiyo yanahitaji bajeti hivyo hupangwa kwa muda mrefu si miezi miwili tu tangu huyo jamaa alivyouliza swali la kebehi bungeni.

Absalom Kibanda said...

Kwa kweli kwa uamuzi huu serikali inapaswa kupongezwa na si Mwakyembe anayetafuta cheap popularity. Mwalimu Nyerere alipata kusema kwamba mtu mwenye akili akishauri upumbavu na wewe ukakubali anakudharau. Mwakyembe anajua kwamba uamuzi wa serikali hautokani na swali lake bungeni bali majibu aliyopewa ni uthibitisho kwamba alichokiuliza kilishaanza kufanyiwa kazi zamani. Mimi sipendi kukubaliana na Mwakyembe kwani anajua kwamba ushauri wake una walakini.

boniphace said...

Mlioko Tanzania namna mnatakiwa kutupanua mawazo zaidi hasa hoja ya kubeza waandishi kama ilivyotamkwa kuwa Mwakyembe kafanya. Sijui kama hansardi zipo mtandaoni nitazitafuta nizisome pia! Kuna siri gani maana mara nyingi huwa natazama hoja na nikiikuta inapigiwa chapuo na Uhuru na hasa ikiandikwa na gazeti jingine lenye mtazamo usio wa kiuhuruuhuru, wa funika kombe? Najawa na mawswali kuliko majibu? Sijamaliza nitarudi nikipata hansard na pia suala la IPTL kumbukeni nalo kulipa umuhimu akina Ngurumo.

boniphace said...

Haya hapa maelezo ya Mwakyembe. Nikirudi tena ni kuongeza chachandu maana hoja hii sasa yafaa ijadiliwe kwa kina na kwa umakini.

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa neno fupi sana, vyombo vya habari ni viungo
muhimu sana kati yetu na wananchi. Nasema hivyo kwa sababu vyombo vya habari
vinatafuta, vinakusanya na kusambaza taarifa na taarifa siyo tu ni mali, vile vile ni nguvu
ya pekee. Lakini vyombo vya habari vikiwa mikononi mwa watu ambao hawana uadilifu,
watu ambao hawaijui taaluma yenyewe ilivyo, ni sawa na kumpa kichaa panga.(Makofi)
76
Mheshimiwa Spika, naeleza haya kwa vile mimi siyo tu mwanasheria vile vile ni
mwandishi wa habari kitaaluma. Yanayotokea hapa yananiuma kweli kweli hasa ya
upotoshaji wa habari. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nasema hivi kwa sababu Rais wa awamu iliyopita alinipa
kazi ya kusimamia ukuaji wa hii taaluma kwa kuwasomesha vijana. Nilikuwa
Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo cha Uandishi wa Habari, Chuo ambacho tumekilea kufikia
mwaka 2003 tukakifanya kuwa Taasisi ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ili waandishi
wetu wasipate tu Certificate na Diploma bali wapate pia Ph.D. kipo pale.
Mheshimiwa Spika, lakini leo naumia moyo kwa nini? Wabunge wako kwenye
semina, waandishi wa habari wenzangu wanautangazia umma kwamba ndiyo Wabunge
wako kule wanatunga sheria kwa kupitia semina. Unapotoa interpretation kwamba
wanafikia maamuzi ina maana tunatunga sheria hata kupitia semina! Mbunge mmoja tu
kati ya Wabunge 324 anasema haoni sababu Mbunge hapigiwi saluti, kesho yake
waandishi wa habari wenzangu wanatoa bold headlines; “Wabunge sasa walilia kupigiwa
saluti.” (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Mbunge mmoja tu anasema yeye angetamani kipindi cha rais
kiwe miaka saba. Hata Wabunge iwe miaka saba. Hajaungwa mkono na mtu mwingine,
lakini kesho taarifa kubwa magazetini zinasema kwamba, “Wabunge sasa wanataka
kujiendeleza kwenye nafasi zao wanataka sasa miaka saba.” Nchi nzima inatuona watu
wa ajabu.
Mheshimiwa Spika, nilitaka tu niseme kwamba huu si uandishi wa habari ila ni
uhandisi wa habari, tunapika habari na wanaofanya haya ni waandishi wachache tu
wanawaharibia jina waandishi wazuri wengi ambao nimekwenda nao shule ni waandishi
wazuri sana. Wakati wa semina Wabunge watatu waadilifu kweli tena tunaowaamini sana
walikuwa wanajenga hoja kwamba Mbunge akiwa kwenye jimbo lake huyo Mbunge kila
msiba lazima achangie. Mtoto yeyote ambaye suruali imechanika au kaptula ya shule
hatatoka kijiji cha mbali basi anakuja kwa Mbunge. Mgonjwa yeyote itabidi apelekwe
kwa Mbunge kwani gari la Mbunge ndiyo ambulance. Hakuna anayechangia mafuta, kila
huduma ya maendeleo Mbunge lazima achangie. Walikuwa wanahoji, sasa jamani na
mshahara wa shilingi milioni 1.2 yote haya Mbunge anabeba. (Makofi)
Kwa nini tusiige utaratibu wa wenzetu wa Kenya na Uganda ambao wana kitu
kinaitwa Constituency Development Fund? Sasa pengine alikuwa nadhani ni
Mheshimiwa William Shellukindo aliongea kwa kiingereza hawakuelewa sasa ikawa
hawa Wabunge wanataka mshahara zaidi, tumepakwa matope nchi nzima. Tatizo ni nini?
Unawa-quote Wabunge out of context. Kwa mwandishi wa habari, this is a crime.
(Makofi)
Tatizo ni nini? Tatizo linaweza kweli kuwa ni la kisiasa lakini vile vile linaweza
kuwa ni la kibiashara. Unajua unapoandika sensational news ndiyo watu wanakimbilia
kununua magazeti kuna ushindani sasa hivi lakini mimi naliona tatizo letu kubwa kwa
77
vyombo vyetu vya habari sasa hivi ni UPE, UPE kirefu chake ni Uandishi Pasipo
Elimu.(Makofi)
Mheshimiwa Spika, Rais wa Uganda Yoweri Museveni alilaaniwa na dunia nzima
alipoamua na kusema sasa nimechoka na upotoshaji. Hakuna kuandika habari bila
Degree ya Chuo Kikuu cha Makerere. Watu wakasema huyu ni dikteta. Sasa tusifikishwe
hapo. Ninachosema tu, ninawaomba Waheshimiwa Wabunge tunao wajibu wa
kuwasaidia waandishi wa habari wapate elimu zaidi.
Naomba pengine kuanzia Bajeti ya mwaka 2006/2007 Waziri anayehusika aweke
angalau scholarship kama 20 kila mwaka, hata 10 kwa ajili ya waandishi wetu wakasome
Chuo Kikuu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, tusipofanya hivyo hawa jamaa wataendelea kutu quote out of
context mpaka dunia nzima itatuona sisi watu wa ajabu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa sababu muda umekwisha kwa kusema naunga
mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)

Absalom Kibanda said...

Ahsante Makene kwa Hansard ambayo nayo imechukua maneno ya mwisho ya Mwakyembe. Kwanza anawafananisha waandishi wa Tanzania na vichaa waliopewa mapanga. Anasema wabunge watatu walizungumzia hilo la nyongeza ya mapato yao tena anasema ni wabunge wanaoheshimika sana.

Sasa Je iwapo anakiri kama anawaheshimu na hoja yao ilikuwa ni hiyo ya kuhoji posho, anakanusha jambo gani?

Mbunge mmoja anatoa hoja ya kutaka wapigiwe saluti katika semina. Sauti zinatoka kwa wabunge wengine 20 na ushee wanapiga makofi ya kuunga mkono, mwandishi anawahoji wengine kadhaa nje ya semina wanakiri kukubali maoni ya mwenzao halafu baada ya mtoa hoja kukaa kimya wabunge wanakaa chini wakicheka na kumpigia makofi. Je wabunge hawataki saluti?

Lakini si hilo tu, mbona hiyo ya kupigiwa saluti kuna magazeti yaliandika 'Mbunge ataka nao wapigiwe saluti' Mwakyembe hakuiona?

Jambo baya kwa Mwakyembe ni kwamba hao waandishi anaowaponda wengi wanatokana na chuo alichokuwa mwenyekiti wa bodi na wengine wanatoka katika gazeti alilokuwa mjumbe wa bodi ambako hakujali kuwatafutia nafasi zaidi za masomo.

Ndiyo maana nikasema msingi wa hoja ya Mwakyembe ulikuwa ni kuwashambulia waandishi na kuwaponda na kidogo akafanya unafiki wa kusema anawapongeza wengi aliosoma nao shule ambao ni waandishi wazuri.

Je Mwakyembe hajui kwamba waandishi aliosoma nao shule baadhi yao ni wahariri wa magazeti yanayoandika habari zinazochapishwa sasa na ambazo zinamkera yeye.

Mwakyembe anajaribu kupotosha kwa kusema kwamba neno maamuzi maana yake ni sheria wakati akijua kwamba si kweli. Hakuna mwandishi aliyeandika kwamba kuna sheria zimepitishwa kwenye semina.

Hivi Mwakyembe hajui kwamba wahariri wengi wa magazeti wanaijua vyema kazi wanayoifanya hata kama kuna wakati wanajikuta wakifanya makosa ya kibinadamu yanayofanywa na wenzao Ulaya na katika nchi nyingine zilizoendelea.

Kwa taarifa yake, Museveni hadi hivi leo analalamika habari kupotoshwa Uganda hata baada ya kutunga sheria ya kuongeza ubora wa viwango vya elimu ya waaandishi. Serikali yake imekuwa ikiendelea kuvitisha vyombo vya habari.

Viongozi wakuu wa serikali Marekani na Uingereza bado wanalalamika taarifa zao kupotoshwa. Je nako huko waandishi hawajasoma?

Waandishi wanajua fika kwamba silaha kubwa ya watu walio madarakani ni kulalamika kupotoshwa kwa taarifa zao kila mara wananchi wanapoinuka na kuwaponda kutokana na kauli walizozitoa katika hali ya uzembe.

Wanaposema wanasimama kifua mbele. Lawama zinapoanza kuelekezwa kwao, wanayageuka magazeti na kudai wamenukuliwa out of context.

Hivi Mwakyembe anaona madai ya kutaka Constituency Development Fund ambayo lazima itakuwa chini ya mbunge siyo njia mbadala ya kujiongezea posho au mapato zaidi?

Au kwa sababu fedha hiyo itakuwa katika akaunti ambayo ni mbunge pekee atakayekuwa na mamlaka ya mwisho juu yake basi Mwakyembe anadai waandishi hawajui Kiingereza. Huku ni kucheza na maneno.

Anonymous said...

Ndugu yangu kibanda,
Baada ya kusoma hansard, hufahamu kuwa waandishi wa habari hasa wasiokuwa na elimu ya kutosha ndio Dr. Mwakyembe anajaribu kuwatetea?.

Unaongea kwa lugha ambayo nadhani si haki kumtuhumu mtu anayechukua muda kuzungumzia tatizo la kada yako, kwanini:
Mwakyembe hakuwafananisha waandishi na vichaa, kama nimemuelewa vizuri alichosema; taaluma ya uandishi, ukiiacha mikononi mwa watu ambao si waadilifu na ambao hawaijui taaluma ni sawa na kichaa kumwachia panga.

Kimsingi,binafsi naiunga mkono kabisa hoja yake wewe kama huiamini angalia mchango wa vyombo vya habari katika mauaji ya Rwanda mwaka 1994.

Unapozungumzia wengi wa waandishi "waliopondwa" na Dr. Mwakyembe wamesoma kwenye chuo kilichokuwa chini ya Dr. Mwakyembe, Ngurumo aliuliza "Makanjanja" wanatokea wapi?

Je una takwimu za kuonyesha ni waandishi wangapi wa habari Tanzania wana Diploma,Digrii, Shahada ya uzamili na Udaktari? kama idadi yao ni ndogo sana huoni kama alichokizungumza Dr. Mwakyembe ni cha maana sana kwa taaluma yako na umma wa Watanzania?.

Uwezo wa kusema kuwa hakuna mwandishi wa habari alisema kuwa maamuzi yanapitishwa kwenye semina, umeupata wapi? kwa ustaarabu ilikubidi umuulize aliyesema akuonyeshe ni wapi amesoma, unaposema hakuna mwandishi aliyewahi kusema. Unaonyesha kuwa unafahamu kila kinachoandikwa na kinachosomwa kwenye vyombo vyetu vya habari kitu ambacho si kweli.

Unapozungumzia makosa ya kibinadamu, inaeleweka, lakini makosa na viwango ni vitu visivyokaribiana hata kidogo. Unapojaribu kufananisha na wahariri wa Ulaya hapo ndipo unapoitia hoja yako mchanga, kwani unaweza kutuelezea vyanzo vya makosa ya "kibinadamu" yanayofanywa kwenye magazeti ya Ulaya na vyanzo vya makosa ya "kibinadamu" yanayofanywa na magazeti yetu, kwa ufasaha?

Unapomkumbusha kuhusu suala la Museveni. kimsingi yeye hakumuunga mkono kwa uamuzi wake, alichosema Dr. Mwakyembe, anaombea Tanzania tusifikie huko.

Nashindwa kuelewa unaposema,CDF ni lazima iwe chini ya mbunge madai hayo umeyapata wapi? CDF ni mifuko ya wananchi wenyewe na siku zote inakuwa chini ya wananchi wenyewe. Tatizo letu watanzania yeyote anayeshabikia kitu kinachotwa "CDF" swali linalokuja vichwani mwetu ni "ulaji" na sio maendeleo, tubadilike!

Nashindwa kukubaliana nawe au nashindwa kuelewa unachojaribu kuzungumza ´mwishoni mwa madai yako unaposema."Au kwa sababu fedha hiyo itakuwa katika akaunti ambayo ni mbunge pekee atakayekuwa na mamlaka ya mwisho juu yake basi Mwakyembe anadai waandishi hawajui Kiingereza. Huku ni kucheza na maneno." Bila shaka unajaribu kumwekea mdomoni Dr.Mwakyembe mawazo yako binafsi,samahani sitaweza kukusaidia kwa hili.

Londo-Helsinki

Anonymous said...

Ndugu Londo,

Nimesoma kwa kirefu na kuchambua majibu yako kwa Bw. Kibanda. Sina la kuongeza kwani maelezo uliyoyatoa na majibu yenye kujitosheleza yanaonyesha ni jinsi gani ulifanya home work yako. Kwa kweli Bwana Londo usichoke kuwaelimisha waandishi wa habari kama kina Kibanda, kile utakapopata nafasi.
Mustapha Abdukadir - TORONTO

Anonymous said...

Boyz ll men sasa kiboko

2006-05-02 16:53:55
Na Mwandishi Wetu, Jijini

Rais Jakaya Kikwete na Waziri wake Mkuu, Bwana Edward Lowassa, marafiki ambao watoto wa mjini waliwahi kuwaita Boyz ll men, wamewadhihirishia Watanzania kwamba hawana mchezo na wamepania kuboresha hali za Watanzania.

Rais Kikwete alidhihirisha hilo jana wakati anahutubia mamia ya wananchi katika kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani, Mei Mosi, Rais Kikwete, sherehe zilizofanyika kitaifa mkoani Shinyanga katika uwanja wa Kambarage.

Katika hali ambayo inaonyesha Rais amepania kutofanya mambo ya danganya toto katika uongezaji wa mishahara na kuboresha maslahi ya watumishi, alitangaza mikakati kadhaa.

Mosi: Alisema ataunda tume itakayotoa hali halisi ya maslahi ya watumishi iliyopo Serikalini na kwenye mashirika ya umma.

Rais alisema tume hiyo pamoja na mambo mengine, itashughulikia uchambuzi wa mishahara na maslahi ya watumishi hao.

Kwa mtaji huo, ’watemi’ Serikalini na katika mashirika ya umma ambao siku zote wanapigania kuongezwa kwa maslahi yao wenyewe, sasa wataumbuka.
Pia madaraja makubwa ya watumishi walionacho na akina pangu pakavu tia mchuzi, yataondoka.

Na kwa upande mwingine, watumishi wasio na nafasi ambao hali zao zimedhoofu kutokana na maslahi duni, watatamba katika uwanja wa haki na usawa.

Rais Kikwete alisema tume hiyo ataitangaza rasmi wiki ijayo na anataka kabla ya mwaka huu kuisha iwe imemaliza kazi hiyo.

Alisema mara baada ya Tume kumaliza kazi na kumpa mapendekezo, hataweka usiku na badala yake atayashughulikia mara moja na kutoa uamuzi juu ya hatua za kuchukua.

Pili: Rais ametaka Mabaraza ya Kisekta ya mishahara ya Kima cha Chini cha mishahara yaundwe mengi ili kushughulikia maslahi ya kundi hilo.

Kwa mtaji huo, kilio cha muda mrefu cha walalahoi huenda kikapungua.
Kwa muda mrefu, wafanyakazi wa kima cha chini wamekuwa wakilalamika kwamba ’wako jangwani’ kutokana na maslahi duni.

Tatu: Rais alisema suala la ajira amelishikia bango na kwamba mikakati inakamilishwa na muda si mrefu Wizara ya Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana italifahamisha Taifa.

Alisema dhamira ya Serikali ni kuongeza ajira kwa Watanzania na kwamba imedhamiria kuweka mazingira mazuri ambayo yatawezesha kukuza ajira nchini ili Watanzania wanufaike na kupunguza dhiki ya maisha.

Nne: Rais pia alizungumzia suala la kuajiriwa kwa wageni katika nafasi ambazo zingeweza kufanywa na Watanzania.

Alisema Serikali itakuwa makini na yenye ukali kwa ajira za aina hiyo.
Kwa kauli hiyo, malalamiko yaliyozagaa kwamba kuna Ma TX feki wanafanya kazi ambazo hata Wabongo ambao hawakwenda shule wanaweza kuzifanya, yatapungua.

Wananchi mbalimbali walioongea na gazeti hili kuhusu hotuba ya Rais walisema serikali ya awamu hii ni kiboko na kama yote yaliyoahidiwa yatatekelezwa, hali za Watanzania zitainuka.

Anonymous said...

Waandishi wa habari wanafanya kazi yao kwa makini. Hebu angalia habari hiyo hapo juu. Sijui Ndugu Kibanda unasemaje?

Khabari hiyo hapo juu imenukuliwa na kuletwa kwenu na F MtiMkubwa Tungaraza.

Anonymous said...

Kibanda,
Hii ni story nyingine angalia jinsi waandishi "wasomi" jinsi wanasababisha majanga.


'Bookman and Aibange are academy, not club coaches'

JEFF Bookman and Ose Aibange are not assistant coaches of two UK Premier league clubs--Chelsea and Tottenham Hotspur--as it had been reported by a section of the local media on Wednesday.

Instead, the two men, who arrived in Tanzania on Tuesday to facilitate a soccer development programme presented by Global Scouting Bureau (GSB), are the coaches of Chelsea and Tottenham Hotspur football academies, respectively.

"It is very unfortunate that some media had not been clear about the status of the two coaches hence causing unnecessary confusion," Elliud Pemba, a close associate of the GSB boss, said.

Pemba also confirmed that both Bookman and Aibange were not Chelsea and Tottenham Hotspur clubs coaches rather coaches of the two Premier side academies that gloom young talent.

Our findings also show that Bookman is the manager of the under-13 team in the Chelsea Football Academy and is not involved whatsoever in training the Premier League side.

Bookman details shows that he is a qualified coach holding an UEFA A Licence Coach, and he also possesses an FA Youth Coaches Award and English FA Coach Educators Award.

The records also show he had also played for Chelsea as a professional player and various non-league semi-professional clubs.

The same is for Ose Aibange, who had previously been with Arsenal FC and the Beckham academy.

However, his name does not appear in line-up of managers of the Premier side, league Tottenham Hotspur.

The GSB vice-president Jack Pemba introduced the two coaches to the media on Wednesday and they were quoted as saying they were highly impressed by Tanzanian national team--Taifa Stars.

At least three newspapers reported yesterday that Bookman was an assistant to charismatic Jose Mourinho of England champions Chelsea.

The 'Daily News', whose phone lines were almost jammed by a barrage of local and international calls demanding clarification on the issue, had decided to dig deeper to clear the air, with success.

The full line-up of the 20 people on Chelsea's club management team, include assistant managers and coaches to Mourinho are Baltemar Brito and Steve Clarke.

Assistant managers are Silvino Louro (Goal keeping coach) and Andre Villas (Assistant coach scout). Others are Rui Faria (fitness coach), Ade Mafe (assistant fitness coach), Mick McGiven (Reserve team coach) and Brendan Rodgers (Youth team coach).

Anonymous said...

Kibanda,
Wewe ni mbabaishaji nini? mbona hujibu hoja za hao jamaa hapo juu?

Anonymous said...

Kibanda hawezi kujibu hoja zenu kwa sababu amejikita katika kujadili MTU. Tukianza kusemana hakuna atakayebaki! Lakini tukikubali kwamba fulani kasema hili au lile, tukalijadili hilo tunaweza kupata mwafaka.

Alilosema Dk. Mwakyembe si jipya. Walishalisema wengi kabla yake. Lakini wengi ama walilisemea kwenye semina, au kwenye magazeti au kwenye vikao vya pombe.

Habari hapa ni kwamba kuna mtu amelisema Bungeni, na anataka litungiwe sheria, serikali iwajibike. Kibanda aseme ni mbunge yupi aliwahi kujenga hoja hiyo (kwa maneno aliyotaka mwenyewe) Bungeni kabla ya Dk. Mwakyembe.

Nimebadilishana mawasiliano na Kibanda kuhusu suala hili, naye amemng'ang'ania Mwakyembe kuwa ni dhaifu. Laiti angeyaweka maelezo yake kuhusu Mwakyembe kwenye blogu yake, au katika mchango huu - maana yale niliyoyaona kwenye blogu yake yamechujwa!

Siku akiniruhusu, nitayabandika hapa, tupate undani wa NAFSI ZAO. Yanaonyesha kwamba anamfahamu Dk. Mwakyembe katika masuala mengi huko nyuma; hakubaliani naye, na ANAMCHUKIA.

Lakini NAFSI ya mtu haikuwa hoja ya wanaharakati. Hapo ndipo Kibanda alipopotea njia.

Absalom Kibanda said...

Nimekuwa nje ya mjadala huu kwa muda sasa. Siyo kweli kwamba nimejikita kumjadili mtu la hasha, bali nimelazimika kulitaja jina la Mwakyembe kwa kuwa yeye ndiye aliyefanywa kuwa msingi wa hoja katika habari ya Ansbert(someni makala ya Ansbert)

Sina sababu ya kumchukia Mwakyembe, lakini nadharau mtu anayetaka kujijengea umaarufu mwepesi (cheap popurarity) ili uonekane kuwa mtetezi wa watu.

Ni jambo la kushangaza kuona watu hawataki watu wapingwe wakati watu hao hao wakitaka kusifiwa.

Mwakyembe anataka kusifiwa kuwa yeye ndiye, wakati akijua kuwa siye mwasisi wa hoja hiyo.

Kuna mtu anasema enakiri kwamba kuna watu wengi waliojadili hoja hiyo kabla ya Mwakyembe lakini hawakufanya hivyo bungeni bali walifanya kupitia vyombo vya habari na katika semina.

NI hoja ya kushangaza na kupuuzwa. Hivi sisi tusiyo wabunge hatuna kibali wala nguvu ya kujenga hoja!

Nina wasiwasi kwamba huenda aliyetoa hoja hiyo tena kwa kujificha jina ni mbunge au anaweza akawa Mwakyembe mwenyewe.

Narudia. Sina sababu ya kumchukia Mwakyembe, ingawa namjua kuwa ni mtu anayependa kusifiwa hata kama sifa hizo hastahili kupewa yeye, tena anatafuta sifa kwa mambo ambayo kimsingi si yake.

Ansbert Ngurumo said...

Nawashukuru wote waliochangia na wanaoendelea kuchangia mjadala huu. Tumeonyesha uwezo, karama na udhaifu wetu. Yote ni sehemu ya ubinadamu. Lakini tukikuza karama na kupuuza udhaifu wetu, tutasonga mbele. Hata hili la Dk. Mwakyembe tunaweza kulitazama hivyo. Na kama nilivyosema awali, tuachane na Mwakyembe tujadili hoja.

Tukubali kwamba serikali ilipotoa majibu ya maandishi kwa baadhi ya hoja za wabunge, Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, Muhammed Seif Khatib, alijibu swali la Dk. Mwakyembe na kui-commit serikali kuwasomesha waandishi. Ndiyo stori iliyoandikwa.

Kibanda hapendi kusikia jina la Mwakyembe lilihusishwa; lakini ndiye aliyejibiwa na serikali. Ushahidi upo. Kama haamini, amuulize waziri mwenyewe.

Na hatuwezi kkubaliana na hoja ya Kibanda kuhusu azima yake ya kuwashambulia watu katika hoja hii. Na kama tutakubaliana naye, hatutaanza na watu wadogo kama Dk. Mwakyembe. Tena kwa kazi na wadhofa wake, anaweza kuwashughulikia wenye tabia hizo asizozipenda. Bahati mbaya anawaogopa kwa kuwa ni wababe na ndio wenye nchi. Yapo mengi maovu yanyofanywa na watawala, hayaandikiki katika magazeti yetu! Tunayaacha hayo, tunamng'ang'ania mbunge mdogo asiye na madaraka; na tunataka kuua hoja ya msingi! Si haki.

Sasa walau tumejua. Serikali imeji-commit kusomesha waandishi. La msingi ambalo sisi wote (akiwamo Kibanda) tunasubiri kuona ni kama bajeti ya serikali italikumbuka hilo. Wajibu wetu si tu kukaa na kuandika hotuba za wakubwa na kuchapisha picha zao. Tuna wajibu wa kuwahoji na kuwawajibisha. Tuna wajibu wa kuwaeleza wasitangulize udhaifu wao katika utumishi. Tuna wajibu wa kuwakumbusha kwamba wajibu wao ni kutumia vema dhamana yao kututumikia.

Nasubiri kuona jinsi Kibanda atakavyowachambua suala hili.

Anonymous said...

Ni kweli la msingi ni kuchambua hoja yenyewe na sio Mwakyembe na wala Kibanda au Londo au Ngurumo.

Kwa mujibu wa hoja ya bwana Mwakyembe ni kwamba waandishi wasiokuwa na elimu ya darasani si waandishi na aliwafananisha hao waandishi na Vichaa na nukuu

"Lakini vyombo vya habari vikiwa mikononi mwa watu ambao hawana uadilifu,
watu ambao hawaijui taaluma yenyewe ilivyo, ni sawa na kumpa kichaa panga".

Je uadilifu na kujua taaluma yako vinahitaji degree? Mimi binafsi sidhani kama ni kweli kama uhandishi unahitaji degree, kwa maana ukiwa na degree haimaanishi kwamba una uadilifu na taaluma. Wezangu humu ndani mnasemaje? Hii sio kebehi na dharau kwa waandishi ambao vile vile Mwakyembe anawatuhumu kwamba nina nukuu

"Mheshimiwa Spika, nilitaka tu niseme kwamba huu si uandishi wa habari ila ni
uhandisi wa habari, tunapika habari na wanaofanya haya ni waandishi wachache tu
wanawaharibia jina waandishi wazuri wengi ambao nimekwenda nao shule ni waandishi
wazuri sana."

Jamani mimi ni mjinga vilevile kama wajinga wengine lakini neno uhandisi kwa kiingereza ni engineering sivyo? Sasa kuna kosa gani waandishi kuzihandisi habari zao? Naona mnataka kunirukia hapa kwa hili!! husifanye hivyo tafakari kwa muda na utakubaliana na mimi kwamba kuna baadhi ya habari zinahitaji kutolewa baada ya kufanyiwa uhandisi. Vile vile kuna kitu kinaitwa Engineering Journalism na waandishi wanapata zawadi katika hili. Sasa kusema hawa jamaa sio waandishi bali na wahandisi si sahii nionavyo mimi.

Je hii inanipa mimi ruhusa ya kumwita Mwakyembe mtu hasiyekuwa na elimu au mlopokaji au hasiyekuwa na taaluma? Nawauliza wezangu? Dennis Londo unaweza kunisaidia hapo kwamba na mimi nawetetea watu kama Mwakyembe wenye upeo duni na elimu ovyo ili waweze kwenda kusoma nje na kuelimika zaidi? kwa sababu mwezangu ndivyo ulivyomuelewa ndugu Mwakyembe nakunukuu

"Ndugu yangu kibanda, Baada ya kusoma hansard, hufahamu kuwa waandishi wa habari hasa wasiokuwa na elimu ya kutosha ndio Dr. Mwakyembe anajaribu kuwatetea?."

Mimi ninatofautiana na Dennis pamoja na Mwakyembe katika hili. Husipokuwa na elimu ya kutosha inamaanisha nini? Kuna haina nyingi za uhandishi wa habari kuna habariza za mazingira, siasa na kadhalika sasa ni elimu hipi ya kutosha wanahitaji?

Kuna haja ya kutofautisha maadili ya uhandishi, makosa ya kibanadamu na kukosa elimu. Sidhani kama hawa jamaa hawana elimu kama anavyodai Mwakyembe, Wengi wa waandishi wamekosa maadili na nidhamu ya kazi na mengine ni bahati mbaya tu huwa yanatokea kama kumnukuu mtu vibaya lakini hili liwe suala la kuwakebehi kwamba hawana elimu ya kutosha, hasa elimu yenyewe inayotiliwa mkazo ni ile ile ya darasani.

Unaweza ukawa na elimu kama Mwakyembe au mwingineo lakini bado ukawa mzembe, dharau, na husio jali. Haya hayaitaji kwenda kusoma nje au kusoma elimu ya juu na kupata stashahada, hapana, haya yanahitaji umahiri, kujali, umakini, uhadirifu na nia. Hivi ni vitu ambavyo haviitaji kwenda Harvad, Sokoine au Mlimani. Ni malezi bora, unyenyekevu, uelewa wa vitu, nia na mwelekeo na mengineyo mengi. Haya yanaweza kumbadilisha Mwakyembe na hao waandishi anawazungumzia kwamba wana matatizo ya uhandishi pasipo elimu (UPE).

Nafikiri ni jambo ambalo linaeleweka kwamba kuna waandishi wengi tu ambao wamesoma na bado hawana uadilifu na kazi zao je hao tuwafanye nini? tuwapeleke wakosomee upadri?

Narudia ndugu Mwakyembe anajenga hoja kwamba hawa waandisi ambao ni UPE wanahitaji kusomeshwa na serikali na sababu ya msingi anayotumia ni kwamba hawa waandisi na wahandishi wamekuwa wakiwa nukuu waheshimiwa wabunge kwa makosa. Tena na mimi napenda kumnukuu kauli yake ambayo na wewe msomaji utakubaliana nami kwamba na yeye vilevile anawajumuisha wabunge wote kwamba huwa wananukuliwa pasipo sahii na wasipowapeleka shule hawa jamaa wataendelea kuwanukuu pasipo sahii. Sasa sijuhi anaposema hawa jamaa anamaanisha wote au waandishi wa UPE peke yake mimi sijuhi. na nukuu

"Mheshimiwa Spika, tusipofanya hivyo hawa jamaa wataendelea kutu quote out of
context mpaka dunia nzima itatuona sisi watu wa ajabu."

Je ni kweli kwamba wabunge wote huwa wananukuliwa vibaya? Si kweli. Je na yeye ni UPE? nisaidieni

Baadhi ya maswali na hoja za ndugu Kibanda ni za msingi ingawa ndugu Dennis anapingana nazo bahadhi. Nitamnkuu Kibanda

“Viongozi wakuu wa serikali Marekani na Uingereza bado wanalalamika taarifa zao kupotoshwa. Je nako huko waandishi hawajasoma? “

"Ndiyo maana nikasema msingi wa hoja ya Mwakyembe ulikuwa ni kuwashambulia waandishi na kuwaponda na kidogo akafanya unafiki wa kusema anawapongeza wengi aliosoma nao shule ambao ni waandishi wazuri."

Nakubaliana na Kibanda hapa ingawa sio moja kwa moja. Kuna dalili kwamba Mwakyembe hana lake jambo, bali ni kutaka kuwaponda tu hawa jamaa. Kama kweli alikuwa na nia ya kuwasomesha kama anavyosema mbona tayari alishafanya hilo. Au anaona hakusikika wakati anafanya hivyo wakati wa Mkapa? hata mimi naanza kuwa na wasiwasi kama ni mkweli na hoja zake, nina mnukuu

"Mheshimiwa Spika, nasema hivi kwa sababu Rais wa awamu iliyopita alinipa
kazi ya kusimamia ukuaji wa hii taaluma kwa kuwasomesha vijana. Nilikuwa
Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo cha Uandishi wa Habari, Chuo ambacho tumekilea kufikia
mwaka 2003 tukakifanya kuwa Taasisi ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ili waandishi
wetu wasipate tu Certificate na Diploma bali wapate pia Ph.D. kipo pale."

Hii kauli kipo pale Chuo na sio tu wasipate Certificate na Diploma bali wapate pia Phd ilikuwa ni pendekezo au inafanyika tayari hapo chuo kikuu? ukisoma vizuri kuna majigambo na maringo katika kauli hii ya Mwakyembe labda ni mimi tu ndio naona hivi.

Suala la Museveni na lazima waandishi wa Uganda wawe na stashahada ya kwanza ili waweze kufanya kazi ya uandishi nahisi inawezekana ndio chanzo cha Mwakyembe kuleta hii hoja bungeni. tofauti na ndugu Dennis Londo alivyomjibu Kibanda kwa kusema kwamba na nukuu

"Unapomkumbusha kuhusu suala la Museveni. kimsingi yeye hakumuunga mkono kwa uamuzi wake, alichosema Dr. Mwakyembe, anaombea Tanzania tusifikie huko."

Na huu ni mfano mzuri wa kunukuu kwa maana katika kauli halisi ya Mwakyembe haipo wazi kuonyesha kwamba anamkanusha Meseveni au anakubaliana naye? Lakini ukiangalia hoja yake ni kwamba anakubaliana na Museveni hila anachoogopa yeye ni kwamba watu wasije wakamwita yeye au serikali madikteta kama wanavyomuita Museveni. Na mimi pia nitamwita Mwakyembe na Serikali dikteta wakisema kwamba lazima kwa mwandishi wa habari kuwa na degree ili kufanya kazi ya uandishi wa habari.

Hili waweke sheria kama hiyo au kuanza kujenga hoja kama hizo lazima elimu ya juu ya uandishi wa habari iwe bure, kwamba kusiwe na kisingizio cha muandishi kusema kwamba sina pesa za kujisomesha. Lakini kwa hali tuliyokuwa nayo Tanzania hali ni bado ngumu hasa ukitilia maanani bajeti ya fedha ya wizara ya elimu.

Uandishi wa habari ni kipaji kama vipaji vingine sidhani kama unahitaji kusoma paka Phd ili kuwa mwandishi wa habari na hata Master si lazima. Dunia ya leo ni tofauti na ya jana mtu anaweza kusoma fani mbalimbali bila kugusa darasa na wala kuonana na mwalimu tunahitaji ubora na sio karatasi linalodai wewe una ubora fulani. Ni jambo zuri kusoma elimu ya juu na kujiendeleza kwa elimu lakini hili tusilifanye kuwa ndio kiada badala ya ziada.

Ninachoogopa mimi ni lini tutaanza kusema ili mtu awe mbunge lazima awe na stashahada ya kwanza ya uongozi au siasa. Ili mtu awe Mzazi lazima awe na stashahada ya elimu ya jamii. Tunaweza kudai haya iwapo tutakuwa na elimu yenye ubora na bure kwa wananchi wetu wote bila kubagua fani. Kuna nchi ambazo zinafanya hivi na bado hawafanyi kuwa lazima katika baadhi ya fani kuwa na elimu fulani hasa ya uandishi.

Makosa yanafanyika na ndio maana watu wanaomba msamaha na waandishi ni binadamu kama Mwakyembe wana fanya makosa lakini tusiwabatize kuwa ni UPE na Vichaa kutokana na makosa yao. Tusijenge matabaka kwamba wale wenye diploma na certificate wakifanya makosa ni kwa sababu hawana degree na wale niliosoma nao mimi ni wazuri kama anavyodai Mwakyembe ndio maana ndugu Kibanda amediriki kumwita Mnafiki.

Tujaribu kuangalia kwa nini maadili ya uandishi yanashuka na sio kwamba wasio na degree ndio wachawi wetu.
Kwa nini watanzania hawana utamaduni wa kusoma magazeti paka kichwa cha habari kiwe Mbunge Afumaniwa au Mbunge atoa Mpya na mengineyo mengi. Tukiyafanyia uchunguzi haya tunaweza tukainusuru kazi ya uandishi na uhandisi wa habari Tanzania.


Haya ni mawazo yangu katika hoja hii. Nikosoeni kwa makosa yangu. Kwa wote niliowataja majina katika maandiko yangu sina nia mbaya wala sina chuki na yoyote. Nia yangu ni kujenga na kuchangia hoja iliyokuwamo na si kingine. Kama nimekosea au nimemkosea mtu basi ni bahati mbaya na naomba unisamhee kwa hilo.

Halifa Mjengwa

My photo
Nimechongwa na mambo haya: Falsafa, Fasihi, Muziki, Habari na Harakati. Sifuati mkumbo. Napenda kuhoji na kudadisi - hulka ya kifalsafa ya kuusaka ukweli - 'UKWELI ULIO UCHI.'