Friday, August 18, 2006

Madaraka ya wanasiasa ni bora kuliko maisha yetu?

Na Ansbert Ngurumo, Toronto

NIKIWA Jijini Toronto, Canada wiki hii, nimekutana na watu wengi mno. Walionigusa zaidi ni watu wawili – Ruby Yang na Thomas Lennon.

Ruby na Thomas ni watengeneza filamu. Hawa ni wanahabari. Wametengeneza filamu inayoonyesha jinsi kutokujali kwa serikali ya China kulivyowasababishia wananchi wengi kupata virusi vya UKIMWI, wakati serikali ikisisitiza kwamba hakuna UKIMWI nchini humo.

Ilikuwa hivi: Miaka ya 1980 na 1990, Wachina walihamasihwa kuuza damu yao kwa vituo vya kukusanyia damu vilivyoanzishwa na serikali ili wapate pesa. Umaskini! Vituo vilivyonunua damu yao viliiuza kwa wenye makampuni na viwanda vya kutengenezea dawa.
Damu nyingine ilizungushwa na kutunzwa katika maabara za hospitali ili itumike kwa wananchi waliohitaji kuongezewa damu. Vifaa walivyotumia havikuwa safi. Na si kila damu ilikuwa safi au salama.

Tangazo kwenye redio na televisheni lilisema: “Nyosha mkono wako, vumilia maumivu kidogo ya sindano; ukunje tena; tayari umeshajipatia Yuan 50.”

Matokeo yake, wananchi waliambukizana UKIMWI. Wazazi wakafa. Watoto wadogo wakabaki yatima. Umaskini ukaongezeka. Serikali kimya!

Likaja tatizo la ziada. Kwa desturi, wachina hawazungumzi mambo yao hadharani. Vyombo vya habari havipewi fursa pana ya kufichua masuala kama hayo. Kuna ugandamizaji mkubwa wa uhuru wa habari. Na watawala wanafurahia hali hiyo.

Ndipo Ruby na Thomas, wakaamua kufanya jambo moja – kutengeneza filamu, ambayo ingekuwa kichocheo cha kusema ukweli ambao serikali haitaki kuusikia. Wakaenda katika jimbo moja la Yingzhou, lililokuwa limeathirika zaidi.

Wakatumia waandishi wachache wenyeji na wanataaluma wengine. Wakatengeneza filamu kali, ambayo sasa imepata tuzo kadhaa za kimataifa. Na imeilaimisha serikali kukubali ukweli!

Filamu hiyo (Damu ya Jimbo la Yingzhou) inaonyesha maisha ya shida ya watoto wa vijiji maskini katika jimbo la Anhui Province. Wanakutana na mambo mawili. Tamaduni zinawazuia kusema ukweli. Na unyanyapaa unaifanya jamii, hata ndugu wa karibu, wawatenge watoto hawa. Hata salamu hawapewi. Kisa? Kila mtu anadhani akiwasaidia naye ataambukizwa. Kifo kinabisha hodi mchanan kutwa. Kila mtu anaona. Hakuna aliye tayari kusaidia. Kisa? Woga wa kifo!

Watengeneza filamu wanaingia kijijini. Wanasalimiana na watoto. Kwa mara ya kwanza, watoto hao wanapata mtu wa kuwashika mkono na kuwagusa!

Mhusika mkuu katika filamu hiyo ni motto aitwaye Gao Jun. Yu mkimya kabisa. Hata akisemseshwa hajibu, hadi mwishoni mwa filamu! Kimya hicho kinawakilisha dhuluma na adha ya raia wengi wasio na mahali pa kusemea katika nchi yao, huku wakigandamiza na maisha duni, matokeo ya uamuzi mbaya wa watawala.

Kutokana na uamuzi huo mbaya, wajanja walianzisha vituo bandia vya kununua damu. Baada ya muda mfupi, maelfu ya wakulima maskini katika jimbo la Henan, walikuwa wameambukiza UKIMWI.

Ghafla, jimbo hilo pekee likasemekana kuwa miongoni mwa watu 280,000 waliouza damu yao, 25,000 walikuwa wameambukizwa virusi miaka ya mwanzo ya 90.

Juzi tukiwa Toronto, mwanaharakati Chi Heng, aliyeanzisha asasi yenye makao makuu Hong Kong kwa ajili ya kupambana na maambukizi yaUKIMWI, alisema China sasa ina watu wapatao milioni moja wenye virusi vya UKIMWI. Wachina wengi walioambukizwa ni wakazi wa vijijini. Huu ni UKIMWI wa kisiasa.

Nguyu ya filamu ya Damu ya Jimbo la Yingzhou nayo ilijadiliwa. Kila mtu aliyesikia habari zao alisifia jitihada za watengenezajiw a filamu hiyo, kwamba zimeibadilisha serikali na jamii ya China. Usiri, urasimu na vitisho vya serikali vilikuwa tishio kwa uhai wa watoto hao.

Sasa wanaishi kwa matumaini. Wanahabari hawa waliona bora wavunje urafiki na serikali ili kuokoa maisha ya masikini na wanyonge, wapiga kura wanaouza damu yao kununua UKIMWI kwa sababu ya umaskini.

Ruby na Thomas, walivunja ukuta wa urasimu na utamaduni, wakatumia taaluma yao kuonyesha uzalendo wao, huku serikali ikiwabeza kwamba wanaichafulia jina katika jumuiya ya kimataifa.

Juzi walipokuwa wakijadili nguvu ya filamu yao, waliifananisha na ya mapanki, - Darwin’s Nighmare ya Hubert Sauper; wakasema ni filamu jasiri inayowatetea wananchi maskini dhidi ya ubabe wa sera mbovu za wanasiasa na matajiri wa ndani na nje.

Wanakemea uzembe wa serikali zetu. Wanataka wanasiasa wasahau kwanza madaraka yao, wakumbatie maisha ya wananchi wao.

Soma vizuri tamko la wabunge wetu kuhusu filamu ya mapanki. Wanafanya kazi kama watu ambao hawakuchaguliwa na wananchi, bali wameteuliwa na rais. Wanadhani lazima wakubaliane naye kwa kila kitu, hata kinachowadhuru wananchi.

Wabunge wetu wanakwepa hoja. Hawaoni wala hawakubali kwamba utandawazi ndilo tatizo. Hawasemi kwamba sera yetu ya uwekezaji ndilo tatizo. Hawakubali kwamba umaskini wa wananchi wetu ndio unawafanya walishwe vitu vya ovyo ovyo.

Zaidi ya hayo, tamko lao na lile la Chama Cha Mapinduzi (CCM) yanafichua pia siri bila kutamka bayana, kwamba sasa wako tayari kuingilia taaluma ya habari. Wanadharau kazi na taaluma za wengine; wanatukuza vyeo vyao.

Wanawabeza waandishi wa Tanzania kwamba ‘wamepotosha’ hotuba ya rais.
Hawajui kwamba waandishi hawa ni watoto wa wananchi wale wale maskini wanaolishwa mapanki, yaliyooza na yasiyooza.

Hawajui kwamba waandishi nao wana macho, pua, masikio na milango mingine ya fahamu wanayoitumia kuandika habari zao. Wanasiasa wetu wanataka kujenga dhana potofu kwamba waandishi ni makarani wa wanasiasa!

Na kwa tabia ya wanasiasa wetu, kama wangekuwa Wachina, wangekuwa wamewafungia watengeneza filamu ya damu eti wanadhalilisha nchi yao, wanatumiwa na watu wasioitakia mema nchi yao. Kwa wanasiasa wetu, nchi ni ya watawala. Kila anayegusa heshima na maslahi watawala anaambiwa haitakii mema nchi yetu! Anaambiwa si mzalendo. Tutabadilika lini?

ansbertn@yahoo.com +255 744 607553 www.ngurumo.blogspot.com

Makala hii inapatikana pia katika www.freemedia.co.tz

Mwisho

1 comment:

Anonymous said...

habari za leo!!!
sikuwa nimesoma makala zako katika magazeti ya hapa nyumbani na hasa gazeti hili la Tanzania.

ni bahati mbaya huwa sisomi gazeti hili lakini baada ya kusoma makala yako ya leo nimejikuta nashawishika kukuandikia.

kikubwa nacho jaribu kukiweka sawa ni kuwa maendeleo yetu hayawezi kupatikana hasa kama halmashuri zetu ambazo kwa dhati na kanuni ndizo hasa zinatakiwa kuondoa kero za wananchi hazitafanya kazi kwa utaratibu

hazina mpango mkakati na utekelezaji. nitaandika mengi lakini nadhani tutapata kwa kuanzia mada zako katika halmashauri na nina uhakika jk atapumua kwa kuzirekebisha


makwasa biswalo
beswallow@yahoo.co.uk

My photo
Nimechongwa na mambo haya: Falsafa, Fasihi, Muziki, Habari na Harakati. Sifuati mkumbo. Napenda kuhoji na kudadisi - hulka ya kifalsafa ya kuusaka ukweli - 'UKWELI ULIO UCHI.'