Monday, October 23, 2006

Natamani waandishi wote wangekuwa hivi

Kama waandishi wote wangekuwa hivi, ni hoja gani imebaki bila kujengwa? Ni nani angethubutu kuchezea taaluma yao? Ni nani angejaribu kuwaweka kwenye kiganja chake na kuwadhalilisha? Ni nani angewakuta wakimshambulia anayewatetea? Lakini upande mwingine unasema, kama waandishi wote wangekuwa hivi, tungewezaje kutofautisha pumba na mchele. Hakika, huwezi kuthubutu kumweka Deus Jovin katika kundi la pumba. Labda kama hujasoma hoja yake hii.

6 comments:

Mjengwa said...

Ansbert!
Umeiboresha blogu yako. Sasa inavutia zaidi. Kazi nzuri!

Reggy's said...

Nimekujibu kupitia blogu yangu. Kuwa 'usimwamshe aliyelala...' Nilikuamsha sana na sasa umeamka; mimi nimelala. Sitakubali, naamka pia, ingawa majukumu yanayonisibu ni mengi, kuliko hapo awali, kuliko...pia mambo mengine

Anonymous said...

Haaa waandishi hapo juu mbona mnatuangusha. Sasa tutamrahumu vipi Harison Mwakyembe na mada yake kwamba kuna waandishi UPE wakati hoja ya Ngurumo hapo juu inajadaliwa visivyo? Jamani Reginald, Maggid na wengine mnakubaliana na Deus Jovin au mnapingana naye? Mnakubaliana na Mwakyembe au ndio mambo fulani? Natumaini waandishi kama nyie mtachangia vizuri hizi hoja badala yake mnatoa salamu na ongera wengine mnataka tuingie kwenye blogu zenu ili tuzisome hoja zenu haya basi tutaingia na humo.

Reggy's said...

Annony naona 'umetutega'. Lakini Nashukuru, kauli yako imenilazmisha kuahirisha safari ya muhimu ili niandike haya machache.

Bahati nzuri, Mr/Ms anony unatufahamu kuwa tuliochangia hapo juu ni waandishi wa habari. Bahati mbaya yawezekana hujui kuwa mimi si miongoni mwa anaowazungumzia Deusdedit Jovin.

Kimsingi nakubaliana naye, Jovin, 100%. Hata hapo nilipoelekeza kwenye blogu yangu ili bwana Ngurumo na wageni wasome, tayari kuna msimamo wangu kuwa 'siwezi kulamba viatu vya chifu'. Kwa msimamo huo, ninamaanisha kuwa naungana na Jovin, kimawazo na kimaneno. Pale nimeeleza kuwa hata wanaopingana na Jovin, kwa maana ya kwamba wanashambulia kile kikaragosi cha Sunday Nation, baadhi yao wanakiri kimoyomoyo kuwa 'kama kikaragosi kile kingechorwa katika gazeti la Tanzania wasingekishambulia. Lakini 'bahati mbaya' kimechorwa na Mtanzania katika gazeti la Kenya. Sioni hoja hapa. Nisichofahamu, yule Mtanzania, Gado, alipewa wazo hilo na wenye gazeti au alichora wazo lake kama mchoraji huru.

Ukweli wangu ni huu: Hatuwezi kuwajumuisha waandishi wote wa Tanzania katika kapu moja la mayai, kwamba likianguka yote yanavunjika, hapana. Wapo makundi mawili kwa kuzingatia hoja iliyopo mbele yetu. Mosi, Wapo 'walioacha kalamu' zao wakati wa kampeni za uchaguzi 2005, wakavaa uanasiasa, upigadebe na uanamtandao. Miongoni mwao, baadhi sasa hivi wamekaa pembeni, wanaweza hata kuikosoa serikali pale inapovuruga, kinamna wametubu dhambi zao, wameokoka. Hawa mimi nimeanza kuwasamehe. Lakini humo humo wapo wale wanaodhani kampeni hazijamalizika, wameziendeleza, wanajiona kama sehemu ya serikali iliyopo madarakani, wengine wameanza kampeni hata za mwaka 2015, wakimfagilia mwanamtandao namba mbili na kuving'oa visiki vinavyoelekea kumzuia. Hawa dhambi yao ni ya mauti, haisameheki.
Pili, wapo waandishi ambao hata kabla ya kampeni, hata wakati wa uchaguzi na leo na kesho msimamo wao uko vile vile, hawa ndio waandishi wa kweli, ndio chaguo langu, ndio model wangu, ndivyo ninavyotaka kuwa, ninavyojaribu kuwa...kama ninashindwa ni mazingira si utashi.
-Uhuru-

Anonymous said...

Lakini hata wewe anonymous, haujaeleweka. Unawaandama hao wachangiaji wawili, Miruko na Majid, mbona hata wewe umeacha hoja ukawashambulia wao bila kutoa ufafanuzi wa hoja iliyowekwa hapo. Naona hapa ni msemo wa nyani haoni 'kundule'. Yawezekana hao wawili waliamua kuzelezea masuala mengine kwa kuwa hawana namna nyingine ya kuwasiliana na ansbert. Bnaada ya kukusema, mimi nachangia, mwamba waandishi wa habari wa Tanzania walidharirishwa kwa kutajwa na katuni ya kenya kuwa wanalamba miguu Rais Kikwete. Wakenya ilikuwa inawahusu nini? Mbona wao hawakuandika wanavyolambva miguu ya Kibaki? Kama unaelewa Daily nation na Sunday Nation yalikuwa yanapingana na utwala wa Moi na kufagilia wapinzani, baada ya kuingia kibaki (upinzani)yaliendelea kufagilia kambi hiyo.

Ansbert Ngurumo said...

Jamani ehe! nashukuru kwa mawazo yenu, Lakini nina hoja. Nyie kina anonymous, si muweke walau email address zenu tuwasiliane? Ndiyo tunahitaji mmawazo yenu, si majina yenu. Lakini kublogu ni kujenga mtandao. Na mtandao wa fikra lazima uwe na mahali unapotua na kuondokea. Twaweza pia kukutana siku moja mahalai fulani tukabadilishana mawazo laivu. Lakini haya hayawezekani tusipofahamiana. Hivyo, basi, mnaonaje na kina anaonymous wawe wanajitambulisha walau kwa email zao kama hawataki tujue majina yao?

Lakini pia, kwa nini wasijitambulishe? Hizi ni enzi mpya. Uhuru wa mawazo uwe wa kweli. Tusimame tuseme. Tuwatazame usoni wale tunaowaambia. Nao watutazame. Tuutazame ukweli, nao ututazame. Ndiyo njia pekee ya kushinda uovu wa fikra na miendendo mibaya inayopandikizwa na wenye mabavu ya fedha au utawala katika jamii yetu. Harakati ni kitu kitakatifu. Tusikionee haya. Hii ni karne ya 21. Si mnajua? Tafadhari, tuendelee kuchangia hoja! ANSBERT

My photo
Nimechongwa na mambo haya: Falsafa, Fasihi, Muziki, Habari na Harakati. Sifuati mkumbo. Napenda kuhoji na kudadisi - hulka ya kifalsafa ya kuusaka ukweli - 'UKWELI ULIO UCHI.'